Skip to main content

TRA Wakomaa na Askofu Kakobe.....Wadai Hawana muda wa Kubishana nae Zaidi ya Kuchunguza Utajiri wake

TRA Wakomaa na Askofu Kakobe.....Wadai Hawana muda wa Kubishana nae Zaidi ya Kuchunguza Utajiri wake

Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), imemuibukia kivingine, Askofu wa Kanisa la Full Gosper Bible Fellowship (FGBF), Zakaria Kakobe, kuhusu utajiri alionao ikisema haina muda wa kulumbana naye, bali inatekeleza maelekezo ya Kamishna Mkuu.

Aidha, mamlaka hiyo imesema haitaki kuwa kwenye malumbano na askofu huyo wakati ikiendelea na uchunguzi dhidi ya vitega uchumi vyake na kuangalia kama analipa kodi ya serikali.

Mkurugenzi wa Elimu kwa Mlipakodi wa TRA, Richard Kayombo, jana alisema maofisa wao wanaendelea kutekeleza tamko la Kamishna Mkuu wa TRA, Charles Kichere, la kuchunguza utajiri wa Askofu Kakobe.

"Sisi (TRA) hatutaki kuwa kwenye malumbano na Kakoke, tulichosema tumeishia hapo. Alichosema Kamishna Mkuu tunaishia hapohapo, hatutakiwi kujibishana naye," Kayombo alisema.

Katika mkutano wake na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam Jumamosi, Kichere alisema mamlaka yake imeipokea kwa furaha kauli ya Askofu Kakobe kuhusu utajiri wake na inataka kujiridhisha vyanzo vya utajiri huo.

Kichere alisema TRA inafahamu kuwa shughuli za kidini hazitozwi kodi, lakini inataka kufahamu kama fedha hizo za Askofu Kakobe zinatokana na sadaka pekee.

Alisema wameamua kuchukua uamuzi huo kutokana na kiongozi huyo wa kiroho kutokuwamo katika kumbukumbu za ulipaji kodi za TRA.

Kauli iliyoleta utata na kuibua uchunguzi huo ni ya Askofu Kakobe kukaririwa wiki iliyopita akidai ana fedha nyingi kuliko serikali na anao uwezo wa kumkopesha waziri pindi akiombwa kufanya hivyo.

Hata hivyo, juzi ikiwa ni siku moja baada ya TRA kutangaza kufanya uchunguzi dhidi yake, Askofu Kakobe alieleza historia ya maisha yake, mali za kanisa na zake na misukosuko aliyopitia na kusisitiza kuwa tafsiri iliyofanyika dhidi ya kauli yake kuhusu utajiri ni ya kimwili na siyo ya kiroho. Alidai kauli yake ilimaanisha yeye ni tajiri wa kiroho na si fedha.

Askofu Kakobe aliishauri TRA kutohangaika naye, badala yake ikatafute fedha mahali kwingine akieleza kuwa ana nyumba moja iliyopo Kijitonyama jijini na aliijenga mwaka 1986 kwa gharama ya Sh. milioni mbili ikiwa ni pamoja na gharama za kiwanja.

Huku akishangiliwa na waumini wa kanisa lake kwenye ibada ya kuuaga mwaka 2017, Askofu Kakobe pia alidai kuwa mwaka 1995 alinunua gari aina ya Nissan Patrol kwa kutumia sadaka za washirika wa kanisa na hivi karibuni waliibuka watu waliochangishana na kumnunulia gari jingine.

Alidai kuwa hata kwao Kakonko, Kigoma hajawahi kujenga hata choo na kilichopo ni makaburi ya wazazi wake waliozikwa kwenye eneo la kuingia kwenye nyumba iliyojengwa na wazazi wao.

Askofu Kakobe pia alidai kuwa kanisa la FGBF ndani na nje ya nchi halina mradi wowote wa kiuchumi kama shamba au hoteli na akasisitiza serikali ichunguze kote huko.

Alibainisha kuwa makusanyo yote ya sadaka huhifadhiwa kwenye akaunti iliyofunguliwa mwaka 1990 katika Benki ya NBC na ni mali ya bodi ya wadhamini ambayo imesajiliwa Wakala wa Usajili, Ufilisi na Udhamini (Rita).

Popular posts from this blog

Jinsi ya kutengeneza SABUNI ya kipande YA KUGANDISHA

Jinsi ya kutengeneza SABUNI ya kipande YA KUGANDISHA Utengenezaji wa sabuni hii una njia nyingi Hatua  ya kwanza Chemsha vipimo 7 vya mafuta ya mawese au mafuta ya shea hadi ifikie hatua ya kimiminika chuja na yaweke kwenye chungu cha mfinyanzi au chombo cha plastiki. Hatua ya pili Pima vipimo 5 vya maji baridi kwenye chombo cha plastiki ongeza kipimo 1cha sodium hydroxide kwa uangalifu mkubwa kwenye maji acha hadi mchanganyiko huo uyeyuke. Subiri mchanganyiko wa sodium hydroxide na mafuta ukaribie kupoa. Hatua ya tatu Taratibu ongeza mchanganyiko wa sodium hydroxide kwenye mawese,huku ukikoroga haraka haraka bila kusitisha ukitumia ubao .hii ni njia nzuri zaidi. Njia ya pili Chemsha mafuta kwenye joto la kadiri ya 55C Changanya maji na sodium hydroxide na uache mchanganyiko huu upoe hadi kufikia joto hilohilo. Baada ya kuandaa mchanyiko wako changanya vimiminika hivyo viwili huku ukikoroga kwanguvu sana kadiri uwezavyo, taratibu sabuni itageuka kuwa laini. Kabla...

Mkuu wa Majeshi mstaafu (CDF), Jenerali George Waitara akemea uwindaji haramu Tarime

Mkuu wa Majeshi mstaafu (CDF), Jenerali George Waitara akemea uwindaji haramu Tarime MWENYEKITI wa Bodi ya Mamlaka ya Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA), Mkuu wa Majeshi mstaafu (CDF), Jenerali George Waitara, amewataka wanachi wilayani Tarime, kuachana na uwindaji haramu, badala yake watumie fursa zilizopo kukuza vipato vyao iii kuondokana na umasikini katika ngazi ya familia.  Pia, amewataka wananchi hao watumie fursa hizo kuwekeza katika miradi na biashara mbalimbali katika maeneo jirani na Hifadhi ya Mbuga ya Serengeti, itakayowawezesha kuwaingizia vipato.  Waitara alitoa wito huo mjini Tarime, juzi, alipokutana na baadhi ya wananchi na kubadilishana nao mawazo, wakati akielekea nyumbani kwake k ij iji cha  Itiry o   kusherekea sikukuu ya Pasaka.  Alitoa ushauri kwa watu wenye nia ya kuwekeza katika miradi mbalimbali ya uzalishaji mali wilayani humo, watumie nafasi hiyo iii kukuza na kuendeleza mji waTarime na wilaya hiyo kwa ...

SADC YALIPONGEZA BARAZA LA USALAMA LA UN KWA KUONGEZA MUDA KWA MISHENI YA ULINZI DRC

SADC YALIPONGEZA BARAZA LA USALAMA LA UN KWA KUONGEZA MUDA KWA MISHENI YA ULINZI DRC 1 2 3 4 5 Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Augustine Mahiga akizungumza na Waandishi wa Habari (hawapo pichani) kuhusu mkutano wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa uliofanyika New York, Marekani na kupitisha Azimio la kuongeza muda kwa vikosi vya usalama vilivyopo DRC. Kushoto ni Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa, Balozi Celestine Mushy. Baadhi ya waandishi wa habari wakimsikiliza Mhe. Mahiga (hayupo pichani). Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na Mwenyekiti wa Kamati ya Mawaziri ya Asasi ya Siasa, Ulinzi na Usalama ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), Mhe. Dkt. Augustine Mahiga (Mb). akihutubia Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa Jijini New York, Marekani. TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki ambaye pia ni Mwenyekiti wa...