Skip to main content

Miaka miwili ya Lowassa nje ya CCM

Miaka miwili ya Lowassa nje ya CCM


Dar es Salaam. Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa leo ametimiza miaka miwili tangu aweke historia ya kuwa kiongozi wa kwanza wa ngazi ya juu serikalini kuihama CCM na anasema hajutii uamuzi wake, yuko imara na licha ya kuzuiwa kufanya mikutano, kura zake zinazidi kuongezeka.

Lowassa alichomoka CCM Julai 27, 2015 ikiwa ni siku chache baada ya Kamati Kuu ya CCM kuondoa jina lake na mengine katika kinyang’anyiro cha urais, uamuzi ambao ulizua mtafaruku mkubwa uliosababisha wajumbe wa Halmashauri Kuu kuimba wimbo wa kuonyesha kuwa na imani naye wakati mwenyekiti wa wakati huo, Jakaya Kikwete akiingia mkutanoni.

Siku moja baada ya kujiengua CCM, Lowassa alitangaza kujiunga na Chadema, chama ambacho kilimpa fursa ya kuendeleza “Safari ya Matumaini” aliyoianzisha CCM, kwa kushirikiana na vyama vingine vitatu vilivyoundwa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa).

Akihojiwa na Mwananchi jana kuhusu miaka yake miwili nje ya CCM, Lowassa alisema pamoja na kupata kura zaidi ya milioni sita za urais, yeye na wapinzani wenzake wanasononeshwa na kunyimwa haki ya kufanya mikutano na kukutana wanachama wao.

Hata hivyo, alipoulizwa ni kwa kiwango gani kunyimwa fursa ya mikutano kumemuathiri, alisema: “Kura zangu zimeongezeka sana, tena sana. Ile tu kutoniona kunaniongezea (kura).

“Nataka kwenda kuwaona (wananchi) lakini siruhusiwi. Nataka kufanya mikutano ya hadhara, siruhusiwi. Sio mimi tu, ni pamoja na wenzangu wote kwenye vyama vya upinzani, hii ndiyo kauli yao.

“Waeleze wananchi na wanachama wa Chadema, nawapenda sana. Natamani kwenda kwao, kuzungumza nao, lakini sipati nafasi.”

Alikuwa akizungumzia amri ya kuzuia mikutano ya hadhara ya wanasiasa hadi mwaka 2020 iliyowekwa na Serikali. Zuio hilo halihusu mikutano ya wabunge na wananchi wao, lakini hawaruhusiwi kualika wanasiasa kutoka maeneo mengine.

Hana lolote la kujutia

Lowassa, ambaye sasa ni Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chadema, alisema pamoja na hali hiyo wanayokumbana nayo, hana cha kujutia kutokana na uamuzi wake wa kujiunga na upinzani.

“Sina cha kujutia hata kidogo,” alisema katika mahojiano hayo yaliyofanyika ofisini kwake jijini Dar es Salaam.

“Nadhani ulikuwa uamuzi sahihi. Baada ya kuutafakari wakati ule na sasa, bado naamini ulikuwa uamuzi sahihi.”

Pamoja na hayo, Lowassa aliyewania urais na kupata kura milioni 6.07 sawa na asilimia 39.97 dhidi ya Rais Magufuli aliyepata kura milioni 8.8 (asilimia 58.46), alisema kuna tofauti kubwa kufanya siasa ukiwa CCM na ukiwa upinzani.

Alisema hali ni tofauti kwa sababu kuna changamoto nyingi zaidi kwenye chama cha upinzani ukilinganisha na CCM.

Alisema kuna maswali mengi ambayo yanajitokeza na CCM ilikuwa na muundo na miundombinu ya kukabili mambo hayo, tofauti na ilivyo kwenye vyama vya upinzani kutokana na uchanga wake.

“Hivi vyama bado ni vichanga, havina capacity (uwezo) kama ilivyo CCM. Kweli kuna changamoto nyingi, leo kuna changamoto hii, kesho kuna hii, lakini kubwa ni kuwahusisha wananchi, tupate nafasi ya kuzungumza na wanachama, kujadiliana nao na kufanya nao kazi kutatua changamoto zilizopo,” alisema Lowassa ambaye alikuwa Waziri Mkuu kuanzia mwaka 2005 hadi 2008 alipoachia ngazi.

Kuhusu Chadema, alisema chama hicho kikuu cha upinzani kinakua haraka, kinaongeza idadi ya wanachama na viongozi wengi, hivyo akasema kinachotakiwa ni kujenga uwezo wao.

Alisema uzoefu huo hauwezi kuja kwa siku moja, bali kwa muda mrefu kama ilivyo kwa CCM.

“CCM ni moja ya vyama vikongwe Afrika na ina uzoefu mkubwa. Ukitulinganisha sisi (utaona) tuko nyuma yao, lakini tunayo majukumu makubwa na makali zaidi mbele yetu kuliko wao,” alisema.

Kuzuiwa mikutano

Akizungumzia changamoto zinazoukabili upinzani katika uendeshaji siasa kwa sasa, Lowassa alisema Watanzania wanajua, wanaona na wanasikia kwamba vyama vya upinzani vinanyimwa haki hiyo.

“Pamoja na kura milioni sita tulizozipata za urais, hatuna haki. Haturuhusiwi kufanya mikutano ya hadhara. Hili ni jambo gumu sana kulielewa. Ni jambo baya sana katika demokrasia,” alisema Lowassa ambaye mikutano yake ya kampeni ilikuwa ikifurika watu kila alipoenda.

“Ni jambo lisilokubalika katika jamii ya kimataifa, lakini imewekwa kwamba ukifanya mkutano wa hadhara unakamatwa unapelekwa mahakamani.

“Sasa hiyo inatunyima nafasi ya kuwasiliana na wanachama wetu. Lakini Katiba ya nchi hii imeruhusu vyama vya siasa vishindane bila kupigana. Tupingane bila kupigana. Vyama vimeruhusiwa kufanya hivyo. Serikali kuzuia mikutano ya hadhara ni blow (pigo) kubwa kuliko zote tulizopata katika uongozi wa vyama vya upinzani.”

Alisema kuzuia mikutano ni kukwaza wananchi.

“Kama hatupati nafasi ya kushindanisha sera zenu, mtakuwa mnawakwaza wananchi na mtakuwa mnakwaza demokrasia katika nchi,” alisema.

Atajwa uchaguzi Kenya

Wakati Lowassa na wenzake wakiwa wamezuiwa kufanya mikutano ya hadhara, jina lake limeibuka kuwa gumzo nchini Kenya ambako kampeni za Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Agosti 8, zinaendelea.

Baada ya kuhudhuria mazishi ya aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Ndani wa Kenya, Joseph Nkaissery, Lowassa alifanya mahojiano na vyombo tofauti vya habari, na tangu hapo amekuwa akitajwa kila mara kwenye majukwaa ya kisiasa.

“Sijisikii lolote jina langu kutajwa Kenya, ila hiyo ndiyo siasa. Mimi ni mwenyekiti wa Malaigwanani (viongozi wa kabila la Wamasai) wa Afrika Mashariki. Kwa nafasi hiyo nina nafasi ya kwenda Kenya kuzungumza na Malaigwanani wenzangu umasaini juu ya nafasi za kisiasa,” alisema Lowassa ambaye anatuhumiwa na wapinzani wa Nasa kumfanyia kampeni Rais Uhuru Kenyatta wa Jubilee.

“Na kule sikuzungumza siasa. Chama changu kilikaa, tukasema kati ya wagombea wote, anayefaa kuliko wenzake ni Uhuru Kenyatta. Ni bora kuliko wengine wote. Baraza Kuu lilitoa kauli ya kumuunga mkono. Kwa hivyo chama kilitoa uamuzi huo na mimi nautekeleza kumuunga mkono Uhuru Kenyatta.”

Upinzani wa Simba, Yanga

Akizungumzia sababu za kufikia uamuzi huo, Lowassa alisema: “Na nieleze, hatukufikia uamuzi huo hivihivi, sisi tuna vigezo vyetu. Tunamwona Kenyatta kama mtu anayependa ushirikiano wa Afrika Mashariki. Pale mpakani Wamasai wanapita kwenda na kurudi kila siku ya maisha yao. Usipompata mtu anayependa ushirikiano huo, mtakuwa mmenoa sana.

“La pili, tunaona katika utawala wake, Kenyatta anapenda, anaheshimu sana wapinzani. Anauona upinzani kama ushindani. Na hiyo ni vizuri, ushindani unatakiwa uwe kama wa Simba na Yanga, sio chuki za kisiasa au chuki za kuuana na kupigana.

“Kwa hiyo nilipokwenda kumzika marehemu Nkaissery, walinialika niseme kidogo, na mimi nikasema ‘msirudi mlikotoka maana ni aibu, nikasema mchague mtu atakayesimamia masilahi ya Afrika Mashariki, mtu ambaye ataheshimu upinzani, mtu ambaye mtakubaliana kufanya kazi naye pamoja na nchi zetu zikawa na amani na utulivu.

“Hayo ndiyo niliyasema, nafurahi yamesikika, najua wamenijibujibu lakini ukweli utabaki palepale. Nawatakia wote kila la heri na uchaguzi uende kwa amani. Amani ya nchi ile ni muhimu sana, amani ikiwapo Kenya, pia itakuwapo Tanzania.”

Lowassa alirudia kauli yake kuwa katika Uchaguzi Mkuu 2020 atashinda kwa kishindo na atakuwa tayari kwa uchaguzi huo, lakini kwa sasa wamwachie Rais Magufuli afanye kazi yake.

“Yapo mambo mazuri anayofanya Rais Magufuli, aungwe mkono. Na kwa kiasi kikubwa anafanya mazuri, lakini haya hayajatoka mbinguni, bali ni wajibu wake,” alisema Lowassa.

“Isionekane kama ni salamu kutoka mbinguni, ni wajibu wake kama Rais. Kazi ya Serikali ni kutoa huduma, ni kujenga shule, ni kujenga hospitali. Ndiyo kazi ya Serikali, kwa hiyo watu wasihesabu kuwa ni hisani.

“Wamefanya kazi yao, kwa kweli nawapongeza, lakini wasionekane wamefanya hisani. Kazi za Serikali zote duniani ni kuleta maendeleo kwa watu au kuandaa mazingira ya kuleta maendeleo.”

Mbunge huyo wa zamani wa Monduli alitoa angalizo dhidi ya siasa za chuki alizosema zimeanza kujitokeza nchini, akisema zisipokomeshwa zitaiingiza nchi pabaya.

Alisema vitendo vya wakuu wa wilaya kushindana kukamata viongozi, wanachama na wafuasi wa upinzani kama njia ya kuwakomoa ni vibaya na havikubali.

Alisema sheria hiyo ya kuweka watu ndani kwa saa 48 iliwekwa kwa ajili ya watu wanaofanya fujo kama kwenye mkutano, lakini si kuwakomoa.

Aliwapongeza viongozi walioamua kuwashtaki wakuu wilaya binafsi waliochukua uamuzi huo, akisema mahakama zina uhuru, zitarekebisha hali hiyo.

Kuhusu wimbi la madiwani wa Chadema kujiuzulu mkoani Arusha na sasa Kilimanjaro, Lowassa alisema ingawa kuhama ni haki yao, inasikitisha kusikia kuna watu wanashawishiwa kwa fedha.

“Wale wanaosema wanapenda sera za Rais Mafuguli, nawatakia heri, lakini si wangesubiri hadi 2020, kuhama ni haki yao lakini waeleze sababu halisi,” alisema.

Source: Mwananchi

Popular posts from this blog

Jinsi ya kutengeneza SABUNI ya kipande YA KUGANDISHA

Jinsi ya kutengeneza SABUNI ya kipande YA KUGANDISHA Utengenezaji wa sabuni hii una njia nyingi Hatua  ya kwanza Chemsha vipimo 7 vya mafuta ya mawese au mafuta ya shea hadi ifikie hatua ya kimiminika chuja na yaweke kwenye chungu cha mfinyanzi au chombo cha plastiki. Hatua ya pili Pima vipimo 5 vya maji baridi kwenye chombo cha plastiki ongeza kipimo 1cha sodium hydroxide kwa uangalifu mkubwa kwenye maji acha hadi mchanganyiko huo uyeyuke. Subiri mchanganyiko wa sodium hydroxide na mafuta ukaribie kupoa. Hatua ya tatu Taratibu ongeza mchanganyiko wa sodium hydroxide kwenye mawese,huku ukikoroga haraka haraka bila kusitisha ukitumia ubao .hii ni njia nzuri zaidi. Njia ya pili Chemsha mafuta kwenye joto la kadiri ya 55C Changanya maji na sodium hydroxide na uache mchanganyiko huu upoe hadi kufikia joto hilohilo. Baada ya kuandaa mchanyiko wako changanya vimiminika hivyo viwili huku ukikoroga kwanguvu sana kadiri uwezavyo, taratibu sabuni itageuka kuwa laini. Kabla...

Mkuu wa Majeshi mstaafu (CDF), Jenerali George Waitara akemea uwindaji haramu Tarime

Mkuu wa Majeshi mstaafu (CDF), Jenerali George Waitara akemea uwindaji haramu Tarime MWENYEKITI wa Bodi ya Mamlaka ya Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA), Mkuu wa Majeshi mstaafu (CDF), Jenerali George Waitara, amewataka wanachi wilayani Tarime, kuachana na uwindaji haramu, badala yake watumie fursa zilizopo kukuza vipato vyao iii kuondokana na umasikini katika ngazi ya familia.  Pia, amewataka wananchi hao watumie fursa hizo kuwekeza katika miradi na biashara mbalimbali katika maeneo jirani na Hifadhi ya Mbuga ya Serengeti, itakayowawezesha kuwaingizia vipato.  Waitara alitoa wito huo mjini Tarime, juzi, alipokutana na baadhi ya wananchi na kubadilishana nao mawazo, wakati akielekea nyumbani kwake k ij iji cha  Itiry o   kusherekea sikukuu ya Pasaka.  Alitoa ushauri kwa watu wenye nia ya kuwekeza katika miradi mbalimbali ya uzalishaji mali wilayani humo, watumie nafasi hiyo iii kukuza na kuendeleza mji waTarime na wilaya hiyo kwa ...

SADC YALIPONGEZA BARAZA LA USALAMA LA UN KWA KUONGEZA MUDA KWA MISHENI YA ULINZI DRC

SADC YALIPONGEZA BARAZA LA USALAMA LA UN KWA KUONGEZA MUDA KWA MISHENI YA ULINZI DRC 1 2 3 4 5 Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Augustine Mahiga akizungumza na Waandishi wa Habari (hawapo pichani) kuhusu mkutano wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa uliofanyika New York, Marekani na kupitisha Azimio la kuongeza muda kwa vikosi vya usalama vilivyopo DRC. Kushoto ni Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa, Balozi Celestine Mushy. Baadhi ya waandishi wa habari wakimsikiliza Mhe. Mahiga (hayupo pichani). Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na Mwenyekiti wa Kamati ya Mawaziri ya Asasi ya Siasa, Ulinzi na Usalama ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), Mhe. Dkt. Augustine Mahiga (Mb). akihutubia Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa Jijini New York, Marekani. TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki ambaye pia ni Mwenyekiti wa...