Skip to main content

Waziri Mkuu Anusa Madudu Minada Ya Madini.......Amuagiza Kamishna wa Madini aende Mererani

Waziri Mkuu Anusa Madudu Minada Ya Madini.......Amuagiza Kamishna wa Madini aende Mererani

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema anafuatilia kwa makini minada ya madini inayofanyika nchini kwa sababu anazo taarifa za kukiukwa utaratibu kwenye minada hiyo.

Amesema ukiukwaji huo unachangia kutobadilika kwa mapato ya mauzo yatokanayo na mnada hata kama kuna vito viliyokakatwa au havijakatwa.

Ametoa kauli hiyo juzi jioni (Jumatatu, Februari 27, 2017) wakati akihitimisha kikao alichokiitisha kwenye makazi yake Oysterbay jijini Dar es Salaam kilichojumuisha Mawaziri wa Fedha pamoja na Nishati, Mkuu wa Mkoa wa Manyara na watendaji wake, Mbunge wa Simanjiro, wamiliki wa mgodi wa Tanzanite One, watumishi waliofukuzwa kazi na wachimbaji wadogo.

Alisema licha ya kuwa Kitengo cha Uthaminishaji wa Madini ya Almasi na Vito cha Wizara ya Nishati na Madini (TANSORT) kinasifiwa kwa kuongeza mapato ya madini, bado kuna kazi ya ziada inabidi ifanyike kwenye minada hiyo ili Serikali iweze kunufainika na madini hayo.

“Uzoefu wa kwenye minada ya korosho unaonyesha kuwa wanaushirika ndiyo wanaiba fedha za wakulima. Nimekuwa ninafuatilia kwa muda sasa uendeshaji wa hii minada na sijaridhishwa na uendeshaji wake. Hakuna tofauti ya bei madini ya Tanzanite yanapokuwa yamekatwa au la,” alisema.

Kwa mujibu wa wataalamu wa madini na vito, inapotokea kuna madini yamekatwa bei inapaswa kuwa juu ikilinganishwa na madini ghafi yanapouzwa moja kwa moja.

Amemuagiza Kaimu Kamishna wa Madini, Bw. Benjamini Mchwampaka (ambaye alihudhuria kikao hicho kwa niaba ya Kamishna wa Madini) aende Mererani na kufuatilia utendaji kazi wa mgodi wa Tanzanite One na suala zima la teknolojia zinazotumika kiwandani hapo.

Waziri mkuu aliitisha kikao hicho kufuatia ahadi aliyoitoa kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika Mererani, wilayani Simanjiro, mkoani Manyara Februari 16, 2017 kwamba akimaliza ziara ya mkoa huo ataitisha kikao na wawekezaji wa Tanzanite One baada ya kupokea malalamiko kwamba hali ya watumishi ilikuwa nafuu wakati kampuni hiyo ilipokuwa inamilikiwa na wazungu kuliko ilivyo hivi sasa.

Ili kuhakikisha ukusanyaji wa mapato katika sekta ya madini unaongezeka, Waziri Mkuu amemwagiza Kamishna wa Mamlaka ya Mapato (TRA) aimarishe ukaguzi kwenye viwanja wa ndege vya Arusha na Kilimanjaro (KIA),

“Kamishna wa TRA na watu wako inabidi mjipange kwa sababu kuna njia nyingi za ukwepaji kodi zinafanyika kwenye sekta ya madini wakiwemo hata hawa wachimbaji wadogo. Simamieni utaratibu wa kufuatilia kodi, nendeni kule walipo, msisubiri waje kuwaletea malipo ofisini. Wasipokuja je? Au wakija wakakuta mmetoka ofisini je?” Alihoji Waziri Mkuu.

Akizungumzia kuhusu uelewa wa sheria miongoni mwa wachimbaji wadogo, Waziri Mkuu alisema Wizara ya Nishati na Madini kupitia kwa Kamishna wa Madini wanapaswa kutoa elimu na uelewa wa kisheria kwa wachimbaji hao ili kupunguza migogoro ambayo imekuwa ikijitokeza kwenye maeneo mengi nchini.

“STAMICO na Kamishna wa Madini fanyeni kazi pamoja, waelewesheni wachimbaji wadogo kuwa uwepo wa vitalu maana yake kuna mipaka ambayo pia inajumisha utoaji wa leseni kwa wenye vitalu hivyo. Kwa hiyo, waelimisheni kuwa mtu hapaswi kwenda upande wa pili wa mtu mwenye leseni, akifanya hivyo atakuwa anavunja sheria.”

“Ninyi ni wadau wakubwa wa sekta hii kwa hiyo mnapaswa kushiriki katika zoezi la kutoa elimu. Mnayo maeneo mengi ya uchimbaji lakini yana migogoro, mfano ni kule Ngaka na Kiwira. Maeneo yote haya yanahitaji usimamizi mzuri. Mnayo Bodi, Mwenyekiti yupo kwa hiyo mnatosha kuifanya kazi hii,” alisisitiza.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amewataka wamiliki wa mgodi wa Tanzanite One waboreshe mahusiano yao na vijiji vilivyo jirani na mgodi huo. “Kuweni karibu na wananchi ili wajue umuhimu wenu na uwepo wenu na waweze kusaidia kulinda mali zenu. Shirikianeni na Halmashauri na Baraza la Madiwani, tangazeni kazi zenu za CSR ili wananchi wajue mmechangia nini katika kusaidia maendeleo yao,” alisema.

Kuhusu suala la watumishi waliofukuzwa kazi kwenye mgodi huo, Waziri Mkuu amemwagiza Katibu Mkuu (OWM-Kazi, Ajira na Vijana), Bw. Erick Shitindi asimamie suala lao na kuwapatia majibu kuhusu hatma ya suala hilo.

Watumishi hao walikuwa wanawakilisha wenzao 201 ambao walifukuzwa kazi Februari 8, 2016 kwa sababu ya kufuatilia maslahi yao vikiwemo malipo ya saa za kazi za ziada (overtime), mishahara ya miezi miwili, malipo ya NSSF, vitendea kazi na usalama wa kazi migodini.

Popular posts from this blog

Jinsi ya kutengeneza SABUNI ya kipande YA KUGANDISHA

Jinsi ya kutengeneza SABUNI ya kipande YA KUGANDISHA Utengenezaji wa sabuni hii una njia nyingi Hatua  ya kwanza Chemsha vipimo 7 vya mafuta ya mawese au mafuta ya shea hadi ifikie hatua ya kimiminika chuja na yaweke kwenye chungu cha mfinyanzi au chombo cha plastiki. Hatua ya pili Pima vipimo 5 vya maji baridi kwenye chombo cha plastiki ongeza kipimo 1cha sodium hydroxide kwa uangalifu mkubwa kwenye maji acha hadi mchanganyiko huo uyeyuke. Subiri mchanganyiko wa sodium hydroxide na mafuta ukaribie kupoa. Hatua ya tatu Taratibu ongeza mchanganyiko wa sodium hydroxide kwenye mawese,huku ukikoroga haraka haraka bila kusitisha ukitumia ubao .hii ni njia nzuri zaidi. Njia ya pili Chemsha mafuta kwenye joto la kadiri ya 55C Changanya maji na sodium hydroxide na uache mchanganyiko huu upoe hadi kufikia joto hilohilo. Baada ya kuandaa mchanyiko wako changanya vimiminika hivyo viwili huku ukikoroga kwanguvu sana kadiri uwezavyo, taratibu sabuni itageuka kuwa laini. Kabla...

Mkuu wa Majeshi mstaafu (CDF), Jenerali George Waitara akemea uwindaji haramu Tarime

Mkuu wa Majeshi mstaafu (CDF), Jenerali George Waitara akemea uwindaji haramu Tarime MWENYEKITI wa Bodi ya Mamlaka ya Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA), Mkuu wa Majeshi mstaafu (CDF), Jenerali George Waitara, amewataka wanachi wilayani Tarime, kuachana na uwindaji haramu, badala yake watumie fursa zilizopo kukuza vipato vyao iii kuondokana na umasikini katika ngazi ya familia.  Pia, amewataka wananchi hao watumie fursa hizo kuwekeza katika miradi na biashara mbalimbali katika maeneo jirani na Hifadhi ya Mbuga ya Serengeti, itakayowawezesha kuwaingizia vipato.  Waitara alitoa wito huo mjini Tarime, juzi, alipokutana na baadhi ya wananchi na kubadilishana nao mawazo, wakati akielekea nyumbani kwake k ij iji cha  Itiry o   kusherekea sikukuu ya Pasaka.  Alitoa ushauri kwa watu wenye nia ya kuwekeza katika miradi mbalimbali ya uzalishaji mali wilayani humo, watumie nafasi hiyo iii kukuza na kuendeleza mji waTarime na wilaya hiyo kwa ...

Bei ya unga sasa ni mara 12 ya mfuko wa Simenti

Bei ya unga sasa ni mara 12 ya mfuko wa Simenti WAKATI bei ya unga wa sembe ikipanda mpaka kufikia kuuzwa kati ya Sh. 2,200 na Sh. 2,500 kwa kilo, ile ya mfuko wa saruji wenye uzito wa kilo 50 imeshuka hadi sh. 9,000, sawa na Sh. 180 kwa kilo. Katika masoko na maduka mbalimbali ya jiji la Dar es Salaam ambayo Nipashe ilitembelea jana, bei ya sembe ilikuwa ikiuzwa kwa kiasi hicho kwa rejareja huku wauzaji wa jumla wakiuza kiroba cha kilo 50 kwa kati ya sh.100,000 na sh.98,000. Ibrahim Omary, mfanyabiashara wa Kariakoo alisema anauza unga wa sembe kwa Sh. 2,400 kwa kuwa hununua kwa bei kubwa kutoka kwa wazalishaji. Alisema kampuni inayojulikana kwa jina la Mkulima huwauzia unga huo kwa Sh. 98,000 na Mama Neema huwauzia kwa sh. 100,000 kwa kiroba cha kilo 50. Kwenye baadhi ya maduka ya kula ya Kinondoni, unga umekuwa ukiuzwa kati ya Sh. 2,200 na Sh. 2,500. Tandika bei ya wastani ni Sh. 2,200, Mwenge Sh. 2,400, Kimara sh. 2,500 na Yombo Vituka sh. 2,200. ...